AFRIKA: Kuongezeka kwa Matumizi ya Simu za Mkononi katika Kupanga Uzazi Susan Anyangu
KAMPALA, Nov 19 (IPS) - Kuongezeka kwa matumizi ya simu za mkononi, hasa katika nchi zinazoendelea, kunawapatia wataalam wa afya aina mpya ya mawasiliano kutoa taarifa za uzazi wa mpango.
"Idadi ya watumiaji wa simu za mkononi inazidi kuongezeka kwa kasi huku idadi ya watumiaji wa simu hizo duniani ikikadiriwa kufikia bilioni 2.6 mwaka 2006 kati ya wakazi bilioni 6.6," anasema David Cantor, meneja ufundi mkuu katika kampuni ya ICF Macro nchini Marekani.
"Takwimu hizi zinatarajiwa kuongezeka hadi bilioni 3.3 au wastani wa nusu ya idadi ya watu wote duniani ifikapo mwaka 2010, huku ongezeko kubwa likiwa barani Asia, Mashariki ya Kati na Afrika."
Cantor, ambaye alikuwa akihudhuria Mkutano wa Kimataifa wa Uzazi wa Mpango mjini Kampala, Uganda Nov. 15-18, anasema kuna ongezeko la nia ya sekta ya afya katika kuwekeza kwenye mawasiliano haya yanayokua kwa kasi.
Kampuni ya One World's Mobile4Good nchini Kenya inatumia teknolojia ya simu za mkononi kuwapa taarifa watumiaji kuhusu fursa za kupima au kupata tiba bure, na pia kutoa huduma ya maswali na majibu ambayo yanaruhusu watu mmoja mmoja kuuliza maswali nyeti ya kiafya.
Nchini Afrika Kusini na Botswana, teknolojia ya simu za mkononi inatumika kukumbusha watu wanaohitaji kupata dawa mara kwa mara.
Jamaica Corker wa shirika la Population Services International (PSI) – programu ya afya ya kimataifa inayolenga katika kupambana na malaria, maisha ya watoto, VVU/UKIMWI na afya ya uzazi – anasema mradi katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo ambako watumiaji wa simu za mkononi wanatumia laini ya bure kupata taarifa zinazohusiana na uzazi wa mpango kumeonyesha nguvu ya teknolojia ya simu za mkononi.
Tangu mwaka 2005, PSI imekuwa ikiendesha laini ya simu za bure ambapo wapigaji wanaweza kuzungumza na waelimishaji na kupata taarifa sahihi kuhusu uzazi wa mpango, au kupelekwa kwenye kliniki au famasi ya karibu, katika eneo ambalo mpiga simu anapatikana.
"Wakati ndiyo inaanza tu, mradi una lengo la kufikia wanawake zaidi, tumeshajifunza kuwa teknolojia ni njia inayofaa kufikia watu kwa ujumbe wa uzazi wa mpango," Corker anasema.
"Kutokana na kwamba wanaume ni idadi kubwa ya watumiaji wa simu za mikononi, wengi wanapiga kwa niaba ya wake zao au marafiki zao wa kike na tunafikisha ujumbe kwao pia."
Matumizi ya laini ya simu za bure ya PSI kwa wanaume wanaotaka taarifa za uzazi wa mpango kunaweza kuonyesha kuongezeka kwa nia ya uzazi wa mpangp miongoni mwa wanaume, pengine kutokana na usiri wa mawasiliano kwa kutumia simu za mkononi.
Kutokana na teknolojia ya simu za mkononi kushuka kwa kasi, Cantor anasema jukwaa limewekwa kwa ajili ya maendeleo ya kasi katika sekta.
Mbali ya kutoa taarifa za uzazi wa mpango, simu za mkononi zinatumiwa kama vyombo vya kufuatilia wagonjwa. Simu za mkononi pia zinatumika kukusanya takwimu za jamii na kliniki, kwa ajili ya kupeleka taarifa kwa wafanyakazi wa afya, watafiti na wagonjwa, na kufuatilia dalili muhimu za mgonjwa. (END/2009)
|
|
|